Saturday 1 August 2015

INASIKITISHA!BABA DIAMOND MBALI NA UGONJWA AFUNGUKA NA KUSEMA HAYA KUHUSU DIAMOND


Baba Mzazi wa Diamond, Abdul Jumaa ‘Baba D’

INASIKITISHA! Wakati mama wa staa wa Bongo Fleva, Nasibu Abdul ‘Diamond Platnumz’, Sanura Kassim ‘Sandra’ akiendelea vizuri baada ya matibabu nchini India, naye baba wa jamaa huyo, Abdul Jumaa ‘Baba D’ anateswa na kansa ya ngozi huku mwanaye huyo akiwa hana habari naye.

Staa wa Bongo Fleva, Nasibu Abdul ‘Diamond Platnumz.

Akizungumza na gazeti hili kwenye mahojiano maalum nyumbani kwake, Magomeni-Kagera, Dar, baba Diamond alisema baada ya kuugua miguu kwa muda mrefu na kumaliza fedha nyingi kwenye hospitali tofautitofauti huku akichanganya na dawa za kienyeji, hivi karibuni amegundulika kuwa ana kansa ya ngozi.

“Miguu imenitesa kwa muda mrefu sana huku ikitoa magamba na maji. Hivi karibuni niliamua kwenda Hospitali ya Ocean Road (Dar) na kugundulika kwamba nina kansa ya ngozi.

LAKI 4 KILA WIKI ZATAKIWA

“Nateseka sana kwani kila baada ya siku saba zinatakiwa shilingi laki nne (400,000) kwa ajili ya dawa, jambo ambalo linaniumiza sana kichwa kwani gharama hizo zimekuwa ni mtihani mkubwa sana kwangu kwa sababu sina uwezo,” alisema Baba D kwa huzuni.

Aliendelea kueleza kwamba, baada ya kugundulika ana kansa aliwasiliana na mwanaye wa kike ambaye naye ni msanii wa Bongo Fleva, Mwajuma Abdul ‘Queen Darleen’ ambaye alimuunganisha na Diamond na kumweleza hali yake juu ya ugonjwa huo.

ATELEKEZWA HOSPITALINI

Alisema kuwa, baada ya kumwambia, Diamond aliahidi kumsaidia katika suala zima la matibabu ndipo akamwambia aende wakakutane katika hospitali hiyo ya Ocean Road.

“Nilienda Ocean Road kama tulivyoelewana na mwanangu Diamond lakini kitu ambacho kiliniumiza ni kwamba nilikaa pale namsubiri kuanzia asubuhi hadi jioni hakutokea, nikaamua tu kurudi nyumbani na kuanzia siku hiyo ‘ameni-bloki’ kwenye simu.

“Kila nikimtafuta simpati na mwanzo tulikuwa tukiwasiliana mpaka nikamtumia na namba ya simu ya daktari wangu. Pia aliniahidi kama itashindikana atanipeleka nje ya nchi lakini yote hayo yameishia hewani, juzi nikasikia amemfanyia sherehe ya bethidei mama yake,” alisema Baba D.

OMBI LA BABA DIAMOND

“Naomba mama Diamond aniambie tu ukweli kama huyo siyo mwanangu nijue kwa sababu nateseka jamani, maana inawezekana alishamwambia mwanaye mimi siyo baba yake ndiyo maana ananifanyia hivi au kama nilimkosea ni kosa gani hilo lisilosameheka?” Alihoji Baba Diamond.

KANSA YA NGOZI

Ugonjwa unaomsumbua Baba Diamond wa kansa ya ngozi ambayo huitwa Melanoma ni ugonjwa unaompa mtu mateso makali kutokana na maumivu anayoyapata na matibabu yake yanahitaji gharama kubwa mno.

Ugonjwa huu huweza kusambaa na kushambulia viungo vingine zaidi ya ngozi kama mifupa na ubongo.

Dalili za kansa ya ngozi ni pamoja na kubadilika kwa ukubwa, rangi au ule muundo wa alama ya ngozi ambayo mtu amezaliwa nao.

Kuna tiba nyingi za kansa ya ngozi. Kuna zile za hospitali ambazo ni lazima zinunuliwe, lakini kuna tiba ambazo kwa ushauri wa daktari hata wewe unaweza kuziandaa bila kutumia gharama kubwa.

Moja ya tiba hizo ni kunywa maji ya moto ambayo yanatibu magonjwa mengi ikiwemo figo, kutoa sumu mwilini, kuyeyusha mafuta tumboni, kurahisisha mzunguko wa damu, kuondoa sumu kwenye ubongo na kusafisha haja ndogo.

TUJIKUMBUSHE

Kabla ya kugundulika kuwa na kansa ya ngozi, Baba Diamond aliwahi kuripotiwa kuwa hoi akisumbuliwa na maradhi ya miguu ambapo pia alilalamika kutelekezwa na mwanaye huyo.

Hata hivyo, baada ya kelele nyingi za ‘midia’, Diamond alikubali kumhudumia kabla ya madai haya mapya kuwa ameingia mitini.

Diamond hakupatikana kufuatia namba yake kutokuwa hewani na hata alipotumiwa malalamiko ya baba yake kwa njia ya WhatsApp hakujibu.

0 comments:

Post a Comment